Na Grace Michael, Tabora
WAGONJWA waliofika na kupata huduma za Madaktari Bingwa ambao wapo
kwenye mpango unaoendeshwa na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya wamefurahia
huduma hizo na kusema kwamba zimeokoa fedha nyingi ambazo wangetakiwa
kuzitumia kusafiri kufuata huduma hizo.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti katika Hospitali ya Mkoa wa Tabora, Kitete,
walisema kwamba ujio wa Madaktari hao umewasaidia kupata huduma nzuri na
zinazohitajika bila ya usumbufu wa aina yoyote na wala kutumia gharama kubwa.
“Kwa upande wangu nashukuru mno kwani nilifika hapa nikiwa na hali mbaya
sana, nilikuwa siwezi hata kula wala kutembea, lakini nipofika na kuonwa na
daktari Bingwa na kunipa huduma nina nafuu kubwa mno kwani naweza kula na
kuzungumza vizuri,” alisema Bw. Shukuru Jumanne (33) Mkazi wa Ipuli mkoani
Tabora.
Mgonjwa huyo alipata huduma ya kutolewa maji kwenye kuta za moyo ambayo
yalikuwa yakimsabishia maumivu makali na kushindwa kupumua vizuri.
Mgonjwa mwingine ambaye naye alipata huduma hiyo, Bi. Halima Juma (49)
mkazi wa Ipuli, Tabora alisema kuwa ana faraja kubwa baada ya kupata huduma
ya kutolewa maji ambapo sasa anaweza kupumua vizuri ikilinganishwa na
mwanzo.
“Sikuwa na uwezo wa kufuata huduma hizi mbali hivyo ujio wa hawa wataalam
kwangu ni kama muujiza, namshukuru sana Mungu kwa kuwaonesha NHIF
mpango kama huu,” alisema Bi. Halima.
Mbali na wagonjwa hawa, pia ndugu wa wagonjwa ambao walikuwa na ndugu zao
wakiwa kwenye chumba cha upasuaji, waliupongeza Mfuko wa Taifa wa Bima ya
Afya kwa kuona umuhimu wa kuleta wataalam hao mkoani Tabora.
Walisema kuwa huduma kama za upasuaji na huduma zingine ambazo walitakiwa
kuzifuata Muhimbili au Bugando wamezipata hospitalini hapa bila ya usumbufu
wowote.
Wamesema kuwa kitendo cha madaktari bingwa kuja mkoani hapo
kimewapunguzia gharama ambazo wangetakiwa kuzitumia, hivyo wameuomba
Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya kuendelea na utaratibu huo ili kukomboa maisha
ya Watanzania wengi wanaoishi katika mikoa ya pembezoni.
Mpaka sasa jumla ya wagonjwa 400 wameonwa na Madaktari Bingwa huku
wagonjwa 25 wamefanyiwa upasuaji tangu zoezi hili lilipoanza siku ya Jumatatu.
Wanachama wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya wakihakikiwa nyaraka zao kabla ya kuingia kupata huduma za Madaktari Bingwa.
Wahitaji wa huduma za kitaalam wakisubiri kuwaona madaktari bingwa.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...