Uelewa finyu juu ya masuala ya utoaji wa mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu
umeendelea kuwa chanzo cha baadhi ya wahitaji wa mikopo kulalamika bila kuanza
kutafuta chanzo cha wao kutopata mikopo hiyo.
Hayo yamebainika hii leo katika ziara ya mafunzo ya wanachuo 147 kutoka Wakala
wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM) unaoendeshea shughuli zake Bagamoyo
mkoani Pwani waliofika Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) kwa
ziara ya mafunzo.
Miongoni mwa maswali yaliyoulizwa na wanachuo hao ni pamoja na uwezekano
wa wafanyakazi kupatiwa mikopo, vigezo vya utoaji mikopo na jinsi ya kubaini
waombaji wa mikopo wenye sifa za kupata mikopo hiyo. Maswali mengine yalilenga
kujua jinsi Bodi inavyowatambua wanufaika wa mikopo ambao mikopo yao imeiva
tayari kurejeshwa.
Awali, Mkurugenzi Msaidizi wa Habari, Elimu na Mawasiliano Bw. Cosmas
Mwaisobwa aliwasilisha mada iliyojumuisha historia fupi ya Bodi, Sera ya
Uchangiaji, Muundo wa Uongozi, Utaratibu wa Utoaji Mikopo na Utaratibu wa
Urejeshwaji wa mikopo ya elimu ya juu.
Akitoa shukrani kwa niaba ya wanachuo hao, Mkufunzi aliyeandamana nao Bibi
Rhoda Samwepa, ameelezea kufurahishwa kwake na jinsi Bw. Mwaisobwa ambaye
pia ni Msemaji wa Bodi, alivyotolea ufafanuzi kwa ufasaha masuala yanayoonekana
kuwa na utata kuhusu mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu na kwamba anaona
umuhimu wa wanufaika kurejesha mikopo hiyo ili wahitaji wengine waweze
kunufaika.
Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu imekuwa ikipokea makundi
mbalimbali ya wadau wa elimu wanaofika kwa lengo la kujifunza masuala ya utoaji
mikopo, vigezo na masharti ya utoaji mikopo na utaratibu wa kurejesha mikopo hiyo
na hivyo kuendelea kuongeza uelewa wa mikopo ya wanafunzi kwa idadi kubwa
zaidi ya wadau.
Sehemu ya wanachuo wa ADEM wakimsikiliza Mkurugenzi Msaidizi wa Habari, Elimu na Mawasiliano Bw. Cosmas Mwaisobwa (haonekani kwenye picha hii).
Baadhi ya wanafunzi wa ADEM wakifuatilia kwa makini mada iliyokuwa ikiwasilishwa na Mkurugenzi Msaidizi wa Habari, Elimu na Mawasiliano Bw. Cosmas Mwaisobwa.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...